MWANAMKENDEGE ; USHAIRI

 hadith hadith njoo
simulizi lake sikio
naanza safisha koo
nikupe langu tukio
eneo nikariakoo
sikujua mwanamkendege

ushungi, umbo na guu
mahabani kazamia
kiunoni kichuguu
moyoni nikaridhia
yalonisibu makuu
sikujua mwanamkendege

tabasamu lake lahaja
nikaona njia nyeupe
amejazia mapaja
si mweusi si mweupe
Radhia jina kataja
sikujua mwanamkendege

lafudhi yake yalamu
tamko lake murua
midomo yake adhimu
kicheko kajaaliwa
kumbe mja haramu
sikujua mwanamkendege

sikujua mwanamkendege
kuuza yake tabia
ucheshi wake nizengwe
pesa kushadadia
ukiwa nacho twende
mwanzoni sikutambua

kwa miguu miwili
nikazama nae hubani
sikutaka subiri
kumfikisha nyumbani
kumbe ndumilakuwili
sikujua mwanamkendege

alianzia kwa kaka
ushemeji kukataa
akasema anataka
nayeye kuzima taa
mwenzenu yamenifika
sikujua mwanamkendege

ndugu kunihabarisha
nimepotea gizani
mie nikakanusha
kwamba haiwezekani
kaka uongo kazusha
sikujua mwanamkendege

sakata jengine bosi
kiongozi wangu kazini
jamani nina mkosi
bosi kazama tegoni
wakayatenda matusi
sikujua mwanamkendege

ajabu kwangu heshima
havui ndio vazi lake
ana aibu kusema
aficha makucha yake
mwanzoni nilimtetea
sikujua mwanamkendege

penzi lake na bosi
mie nijulie wapi
huyu binti mkosi
sijui ana mangapi
nahisi ana virusi
sikujua mwanamkendege

uzuri wake hadaa
mwepesi wakulaghai
mie hadi nashangaa
kumuacha mpenzi zai
kwake hadi kukaa
sikujua mwanamkendege

Tamaa yake si pesa
hata ukiwa na mvuto
utaanzaje kumtosa
jinsi alivyo mrembo
utulivu ndio kakosa
masikini mwanamkendege

Mwengine rafiki yangu
tamaa ikamuingia
falagha chumbani kwangu
shemejie kamuingia
meona kwa macho yangu
hakika mwanamkendege

Kaiponza kazi yangu
bosi aliponogewa
kafuta ajira yangu
apate kumchumbia
masikini moyo wangu
kauponza mwanamkendege

Sihadaike na uzuri
uzuri gamba la nje
fukuto huwa uturi
harufu isikuponze
maisha ni sura mbili
sikujua mwanamkendege


 usiku uingiapo
nyota hupendezea
kwa ule wake mweko
lakini mchana jua
nisawa mwanamkendege