UTENZI WA MAHABA

''Zawadi ni chachu ya mahusiano ya aina yoyote ile, mzawadie ulicho nacho yule ambaye unahisi ni sahihi kuzawadiwa nae, naamini tabasamu lake usoni ni ishara tosha yakufarijiwa na zawadi uliyompa, kuna aina nyingi za zawadi, lakini katika mapenzi Maneno matamu ni zaidi ya zawadi zote unazozijua wewe, waswahili huamini NENO HUUMBA......''

UTENZI WA MAHABA
Na
Bin Zongo
leo nachana kifua
nautoa moyo nje
nataka kuyaachia
yalo ndani uyaone

si joto wala baridi
ni wastani kipupwe
leo nataka kuahidi
ukweli wangu nikupe

kupenda kama umbea
masuto nastahili
naapa sitokimbia
majivu ntayakubali

laa kupenda ni homa
matibabu weka mbali
nataka kuumwa homa
joto mwili liwe kali

mapenzi kama ugali
mpunga mie wanini
sitaitaka zohari
mahindi weka chumbani

kupenda jambo geni
sijawahi kabla yako
naapa kwa rahmani
nafsi yangu mali yako

mwenzako kwetu pwani
kudekeza nimefunzwa
kuoga nawe bafuni
Tanga nimesisitizwa

kupiga ni ukatili
uuaji na ujangili
ili niwe kamili
nimeaswa kukujali

mie kwako zawadi
nitunze nitakufaa
nitatimiza ahadi
hutaikata rufaa

sharti langu moja
tulia na ujiheshimu
usije leta vioja
eti hakuna ushemu

urembo wako shani
kumbuka ni mali yangu
tulia nao nyumbani
siuze kilicho changu

mahaba niache hai
ukiniua utanionea
kuwa nawe najidai
upendo wangu pokea

uongo ni msongo
uambae utanitesa
usije shiriki hongo
mwili wako si kipusa

heshima maji baridi
nipe nipoze koo
kiburi kisikuzidi
nisije kusema poo

pesa sio mapenzi
kama ndio ntakuhonga
ubahili sitaridhi
wakati nimeshapenda

matani machombezo
kufinyana ni mchezo
weka mbali mawazo
mahaba yangu tulizo

niite kwa jina langu
lafudhi weka ya pwani
zijue hisia zangu
faraja nipe chumbani

mwengine atoke wapi
kwako nimesharidhika
mitala wala sitaki
mapenzi sio shirika

mapenzi kama ni tenzi
nunua kabisa zeze
usiifanye ajizi
pokea huu utunze.
Na.
BIN ZONGO

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »