Tafakari Wengine

Muda mwingi hua unautumia kutafakari mazuri yako huku ukihitaji kusifiwa, hua unatamani kuongelewa wewe tu, unatamani kuonekana  Na wote wanaokuzunguka wasifu nakukuheshimu.

 Ni nadra sana mtu kutoa nafasi yakutafakari wengine, hivi ndivyo tulivyoumbwa, tumeumbwa na umimi.

Unajiona Bora kuliko wengine, wewe ndio unajiona mwenye akili, busara Na ushauri mzuri unaweza kutokea kwako.

Ni ajabu sana tabia hii Na kwa vile ni asili ya kuumbwa kwako sina lawama katika hilo

Ila leo nataka utenge muda kutafakari wengine, kuona vipawa vyao, nafasi yao, akili zao Na tamaa zao.

Ndio,

Anza sasa kumfikiria mtu wako wakaribu, ana umuhimu gani kwako.

Acha kuwaza wewe tu ndio mwenye umuhimu kwake.

Jiulize maswali ya Je ni vipi ingekuwa kama yeye asingekuwepo.

Tuanze Na msaidizi wako wa kazi za ndani.

Yeye anafua nguo zako, anakupikia, anakufanyia usafi wa nyumba n.k.

Acha kiburi chakusema hata kama asingekuwepo ungetafuta mwengine fikiria kuna watu duniani wanatafuta msaada kama huo lakini hawaupati.

Hivi unadhani fedha yako unayomlipa inazidi wema wakukutunzia nyumba yako, vitu vyako Na wakati mwengine hata watoto wako??

Tafakari wengine!

Kila mtu aliyekuzunguka anamchango mkubwa kwenye saikolojia yako.

Hebu pata picha unaamka asubuhi halafu kila unayekutana nae unamsalimia halafu anakujibu hovyo nakukudhalilisha au wengine hawakujibu wanakutema mate.

Unadhani saikolojia yako itakuwa nzuri hali hiyo ikiendelea mpaka unafika kazini kwako?

Wafanyakazi wenzako wote hawakupi ushirikiano hata wasalamu, kila mmoja anakuchunia nakukuona silolote.

Shtuka rafiki!

Kila mmoja unayekutana naye barabarani ana Faida kwako, ukijiheshimu atakuheshimu Na wewe utajisikia vizuri kuheshimiwa.

Leo nataka utafakari umuhimu wa kila aliyekuzunguka hata yule jamaa mtaani ambaye huna mazoea nae, husalimiani nae wala humkubali.

Nayeye ni sehemu ya maisha yako, anza sasa kuwaza umuhimu wake.

Paulo Coelho kwenye kitabu chake cha the alchemist kuna mahali anasema katika maisha yako yakawaida yule unayekutana nae kila siku ujue ni sehemu ya historia ya maisha yako, ni muhimu kumthamini sababu ana mchango mkubwa kwako.

Ni sahihi mtazamo wa bwana Coelho namimi nipigilie msumari hakuna ambaye hana mchango kwako, hata adui.

Wanasema wataalamu wa mambo ili ufanikiwe unahitaji marafiki lakini ili ufanikiwe zaidi unahitaji maadui.

Nakamilisha Na mfano wakubuni ambao naamini utaona Faida za maadui kwenye maisha yako.

Bosi mmoja alikuwa anapata malalamiko kila siku kuhusu mfanyakazi wake, alikuwa anaambiwa hafai, mla rushwa mara ooh hathamini wateja.

Ilifika mahali maneno kuhusu mfanyakazi wake yalimkera akataka kumfukuza kazi ila kabla hajafanya ivo akaenda kuomba ushauri kwa Mzee wake ambaye ndiye aliyemkabidhi ofisi.

Mzee akashtuka sana kusikia maneno anayoambiwa mwanae kuhusu mfanyakazi yule.

Alishtuka sababu yeye alimfahamu vema mfanyakazi yule.

Mara kadhaa wakati wa uongozi wake alishapata barua kutoka kwa wateja wa kampuni wakisifu huduma za mfanyakazi yule.

Wengine walidiriki hadi kumuomba akafanye kazi kwenye kampuni yao, lakini Mzee alikataa.

Mzee kwavile alimuachia mwanae ofisi akamwambia hatampa mbinu yoyote ya uongozi kwasababu anaamini kijana wake atakuwa mbunifu Na atakuwa Na mbinu mpya kwa maendeleo ya kampuni hivyo alivyotakiwa kutoa ushauri akatabasamu tu kisha akamwambia mwanae.

"Ni vema ukasikiliza maneno ya watu sababu lisemwalo lipo lakini vilevile ni vema ukachuja unayoambiwa maana Mti mwema mara zote ndio huandamwa kwa mawe"

Bosi alipoyatafakari maneno ya Mzee wake akayaelewa nakuona kuna haja yakuanza kufatilia utendaji kazi wa yule mfanyakazi kabla yakumfukuza.

Loh alipoanza kumfatili ndipo alipoanza kukutana Na sifa lukuki kuhusu utendaji kazi wa mfanyakazi yule.

Bosi akamuweka karibu zaidi nakumuongezea mshahara.

Maadui waliokuwa wanamchonganisha walisababisha jamaa ijulikane thamani yake.

Mwisho wa mfano huo.

Naomba uruhusu milango yako yote ya fahamu itafakari umuhimu wa yeyote uliye naye karibu kisha mthamini, muheshimu Na umjali.

Tambua yakwamba binaadamu tunategemeana katika kukamilisha tamaa zetu zote.

 Na
Omar ZONGo
SIMULIZI ZINAISHI

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »